Alfonso Maria wa Liguori
From Wikipedia, the free encyclopedia
Alfonso Maria wa Liguori (Marianella, leo katika jiji la Napoli, nchini Italia, 27 Septemba 1696 - Nocera de' Pagani, katika wilaya ya Salerno, 1 Agosti 1787), pamoja na kuwa mtawa na padri mwanzilishi wa shirika la Mkombozi Mtakatifu sana, halafu askofu wa Kanisa Katoliki, anajulikana kama mwanateolojia wa maadili, mwalimu wa maisha ya Kiroho kwa wote, hasa watu wa chini, mwandishi wa vitabu vingi sana, mwanashairi, mchoraji na mwanamuziki.
Alikuwa kielelezo cha mchungaji mwenye ari na wema katika kutangaza Neno la Mungu na kuadhimisha sakramenti ili kuokoa watu, akitia maanani hisia na miguso, si hoja za akili tu, ili kuwaelekeza wawapende Mungu na majirani[1].
Alitangazwa mapema na Papa Pius VII kuwa mwenye heri tarehe 15 Septemba 1816, halafu Papa Gregori XVI alimtangaza mtakatifu tarehe 26 Mei 1839, na Papa Pius IX kuwa mwalimu wa Kanisa mwaka 1871. Yeye tu alipewa cheo hicho kabla ya miaka mia tangu afe.
Sifa hiyo ilimfaa kwa sababu nyingi, hasa utajiri wa mafundisho yake kuhusu maadilidini yaliyotoa sawasawa msimamo wa Kikatoliki, hivi kwamba Papa Pius XII alimtangaza pia msimamizi wa waungamishi na wa wanateolojia ya maadili.