Papa Fabian
From Wikipedia, the free encyclopedia
Papa Fabian alikuwa Papa kuanzia mwaka 236 hadi kifodini chake tarehe 20 Januari 250[1]. Alitokea Roma, Italia.
Alimfuata Papa Antero akafuatwa na Papa Kornelio.
Alichaguliwa akiwa bado mlei[2], akatoa mfano mtukufu wa imani na maadili.
Aliongoza Kanisa miaka mingi katika hali ya utulivu, hasa chini ya kaisari Filipo Mwarabu ambaye anasemekana alibatizwa naye[3].
Kadiri ya wanahistoria Wakristo[4][5], chini ya kaisari Decius (250 BK), Papa Fabian alituma maaskofu 7 kutoka Roma kwenda Gallia (Ufaransa wa leo) wakahubiri Injili: Grasyano huko Tours, Trofimo huko Arles, Paulo huko Narbonne, Saturnini huko Toulouse, Denis huko Paris, Austremoni huko Clermont na Martial huko Limoges.
Hatimaye alifia dini yake katika dhuluma ya kaisari Decius. Sipriano wa Karthago alisifu ushindi wake na kwamba alitoa kielelezo bora cha uongozi[6].
Tangu kale anaheshimiwa na Wakatoliki na Waorthodoksi kama mtakatifu mfiadini[7].
Sikukuu yake ni tarehe 20 Januari[8].